Mtanzania Aliyedaiwa Kumuua Mkewe kwa Visu London, Full Story


SIMULIZI ya Mbongo aliyetajwa kwa jina la Belly Kasambula (38), kudaiwa kumuua mkewe, Leyla Mtumwa almaarufu Ndaya (36), wote raia wa Tanzania, inatisha, Ijumaa Wikienda lina full story.

TUJIUNGE LONDON, UINGEREZA

Tukio hilo la kusikitisha lilijiri usiku wa kuamkia Ijumaa iliyopita ya Machi 30, mwaka huu katika nyumba wanayoishi Watanzania hao iliyopo eneo la Haringey, Kirkstall Avenue, N17 jijini London nchini Uingereza.

GLOBAL TV LONDON

Mwakilishi wa Global TV Online aliyeko jijini London, Amuri Musema alilihabarisha Ijumaa Wikienda kuwa, mauaji hayo yalijiri baada ya kuzuka ugomvi baina yao.

Kwa mujibu wa Musema, ilikuwa muda mfupi baada ya Leyla kurejea nyumbani akitokea disko la usiku alikokuwa amekwenda na marafiki zake.

Musema alisema kuwa, polisi walipofika nyumbani hapo walikuta tayari mwili wa Leyla upo chini akiwa ameshafariki dunia.

Taarifa nyingine zilisema kuwa, mara baada ya tukio hilo, rafiki wa Leyla ambaye alikuwa naye klabu aliyejulikana kwa jina moja la Mecky ambaye naye ni Mtanzania ndiye aliyethibitisha kutokea kwa tatizo hilo.

WARUDI WAKIWA WAMELEWA

Ilisemekana kuwa, Leyla na Mecky walikuwa klabu ambapo walijirekodi wakicheza Wimbo wa Ojuelegba wa mwanamuziki WizKid wa Nigeria ambapo walirudi nyumbani wakiwa wamelewa.

Kwa mujibu wa majirani, Leyla alipofika nyumbani alimkuta mumewe huyo akimsubiri ambaye alianza kufoka na kutukana, jambo lililoibua ugomvi mkubwa kati yao.

MECKY AONDOKA

Baada ya mzozo huo kuwa mkubwa, Mecky aliondoka zake ndipo jamaa huyo akadaiwa kuanza kumshushia kipigo kisha kumchoma visu mbele ya mtoto wake wa miaka 12.

Ilielezwa kuwa, mtoto huyo Leyla alimzaa na mumewe wa kwanza ambaye ni raia wa Nigeria.

POLISI WAFIKA

Ilielezwa kuwa, ilipofika majira ya saa 1:30 asubuhi, hali ya Leyla ilikuwa mbaya hivyo mtoto wake huyo wa miaka 12 alipiga simu katika kitengo maalum cha polisi cha makosa ya jinai (Met’s Homicide and Major Crime Command) cha London na kuwajulisha juu ya tukio hilo.

Baadaye kitengo hicho cha polisi kilitoa taarifa yake kwamba kilipofika nyumbani hapo kilimkuta Leyla akiwa ameshafariki dunia na mwili wake ukiwa na majeraha ya visu.

Polisi hao walisema kuwa, baada ya kumkuta katika hali hiyo, walimchukua kwa ambulance na kumpeleka hospitalini.

LEYLA AKATA ROHO

Hata hivyo, pamoja na jitihada hizo za polisi kuwahi eneo la tukio na kumchukua kisha kumkimbiza hospitalini walipofika waliambiwa ameshafariki dunia, lakini Leyla aliaga dunia majira ya saa 2:11 asubuhi kwa saa za London.

Katika tukio hilo, polisi wanaendelea na uchunguzi wa tukio hilo huku wakimshikilia mwanaume huyo ambaye ni mtuhumiwa namba moja.

Katika taarifa yao, polisi hao walitoa namba zao za simu ili kama kuna mtu yeyote anayewafahamu Leyla na Belly, basi atoe taarifa kwao kwa ajili ya kujua nini cha kufanya.

BAADA YA KIFO SASA

Kama ilivyo desturi ya mitandao ya kijamii, mara baada ya kujiri kwa tukio hilo, kila ukurasa wa kijamii uliwekwa taarifa zake juu ya tukio hilo hivyo Ijumaa Wikienda likaingia mitaani kusaka ukweli.

Kwa mujibu wa vyanzo vya uhakika, Leyla ni mwenyeji wa Kaloleni jijini Arusha wakati Belly ni mwenyeji wa jijini Dar.

HIDAYA WA PEPE KALLE

Taarifa hizo zilieleza kuwa, Leyla ni mtoto wa mama mmoja maarufu jijini Arusha aitwaye Hidaya aliyeimbwa na mwanamuziki wa Kongo, marehemu Pepe Kalle katika wimbo wake wa Hidaya wa miaka ya 1990 kwa kuwa alikuwa ni mwanamke wa shoka aliyekuwa na fedha nyingi.

Kwa upande wake Belly naye alidaiwa kuwa ni mtoto wa mwanamuziki mkongwe wa dansi nchini, Skasi Kasambula hivyo ngoma kuwa droo kwani wote ni watoto wa mastaa.

TWENDE KALOLENI, ARUSHA

Baada ya kuwepo kwa taarifa hizo, Ijumaa Wikienda lilifika nyumbani kwa Hidaya, Kaloleni jijini Arusha ili kujua undani wa tukio hilo na kukutana na vilio na simanzi nzito.

Ijumaa Wikienda lilipofika nyumbani hapo mchana wa Jumamosi iliyopita lilikuta tayari kumefungwa maturubali kuonesha kuwa kuna msiba.

Akizungumza na Ijumaa Wikienda, kaka wa Leyla aliyejitambulisha kwa jina la Abdul Mtumwa alisema ndugu, jamaa na marafiki wamefikwa na msiba mzito ambao umetokea kwa mtu aliyependwa na wengi.

NI MSHTUKO

Huku akiomba kuachwa kwanza atulie na kupanga taratibu za kinyumbani, Abdul alisema kuwa, baada ya kupata habari hiyo ya mshtuko, walikuwa wakisubiri taratibu za kiuchunguzi za Uingereza zikamilike marehemu aletwe nyumbani Arusha kwa mazishi.

TAARIFA KAMILI NI LEO

Alisema kuwa, wanachokifanya kwa sasa kama familia ni kuwasiliana na mjomba wa Leyla ambaye naye yupo nchini Uingereza kwa ajili ya kuwapa taarifa kamili ya kinachoendelea ambapo utaratibu wote utatolewa leo nyumbani hapo.

“Ni mshtuko kila kona, kila mtu amepata mshtuko kama unavyoona, watu wanalia, hawaamini wanachokisikia. Hata hivyo, taarifa kamili kuhusu msiba huu tutatoa Siku ya Jumatatu (leo),” alisema Abdul.

TURUDI LONDON

Kufuatia tukio hilo, mwakilishi wa Global TV alisema kuwa, Leyla ni maarufu hivyo kila mtu alishtsuhwa na taarifa hizo.

“Hapa London hali ni ya taharuki, kwa wanaomjua Leyla alikuwa mtu mwenye heshima sana hivyo kila mtu ameguswa kwa namna yake.

“Habari zinasema kuwa huyo mwanaume alifunga ndoa na Leyla mwishoni mwa mwaka jana hivyo kila mtu huku aliwajua kama mke na mume,” alisema ripota huyo wa Global TV
xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

https://www.youtube.com/watch?v=_NaWOSR1kR8

https://www.youtube.com/watch?v=eNIp3tDBKLg

https://www.youtube.com/watch?v=IQ6TLEsHRe8