Hekaheka:MAMA DIAMOND AKILI KUMPIGA HAMISA MOBETO KISA HIKI HAPA


Sanura Kassim ‘Sandra’

BAADA ya kuvuma kwa taarifa mitandaoni kuwa mama wa staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, Sanura Kassim ‘Sandra’ amempa ‘vitasa’ mwanamitindo Hamisa Mobeto, Ijumaa limemtafuta bi mkubwa huyo na kufanya naye mahojiano maalum (exclusive) ambapo amefungukia sakata hilo kwa kirefu.

Mama Diamond alifungukia hilo la kumpiga Mobeto ambaye amezaa mtoto mmoja na mwanaye, Jumanne iliyopita katika mahojiano maalum yaliyofanyika katika duka la bintiye, Esma Khan ‘Esma Platnumz’ lililopo maeneo ya Afrika Sana jijini Dar.
ISHU ILIPOANZIA
Mama Diamond alisema ishu hiyo ilianzia Mei 13, mwaka huu mara baada ya yeye pamoja na Diamond kutoka kwenye shoo ya msanii wa Kundi la Wasafi Classic Baby (WCB), Mbosso.

Alisema, kwa kuwa walirudi nyumbani kwao Madale usiku, yeye alilala katika chumba chake bila kujua Diamond amelala na Mobeto chumbani kwake.

KULIPOPAMBAZUKA
Bi mkubwa huyo alisema, kulipopambazuka, alikwenda kwenye mishemishe zake na aliporejea ndipo alipoliamsha dude baada ya kushtukia mrembo huyo amelala nyumbani hapo.

MAHOJAINO KAMILI YALIVYOKUWA

Ijumaa: Hivi hizi tetesi za kumpiga Hamisa, mpaka kumvua wigi ni za kweli au uzushi tu?

Mama Diamond: Uzushi wa kivipi? Ni kweli.

Ijumaa: Kwa hiyo ni kweli ulimpiga?

Mama Diamond: Ndiyo na wigi nikamvua.

Ijumaa: Kwa nini sasa ulimpiga na ni mzazi mwenzie na mwanao?

Mama Diamond: Hayo mambo ya mzazi mwenzie ni huko, pale Madale ni kwangu na simtaki nyumbani kwangu kabisa.

Ijumaa: Kuna kosa lolote alishawahi kufanya kwako labda?

Mama Diamond: Kitendo cha kuniitia mimi Shilawadu (kipindi cha udaku cha Televisheni ya Clouds) kilinikera sana halafu nikaanza kutukanwa kwenye mitandao ya kijamii.

KWA NINI KILIMUUMA?
Kwa muda mrefu mashabiki wa ubuyu Bongo walikuwa hawajui kiini cha ugomvi wa mama Diamond na Mobeto lakini sasa ameweka bayana.

Iko hivi, mapema mwaka jana, wakati Hamisa alipokuwa amenasa ujauzito wa Diamond ambaye wakati huo alikuwa kwenye uhusiano mzito na Zari, walikubaliana kufanya siri jambo hilo ili Zari asiusome mchezo.
Mama Diamond inaonekana alikuwa kwenye huo ‘mpango mkakati’ wa kuficha ujauzito wa Mobeto hivyo kitendo cha kuwaita Shilawadu wamshuti alipokwenda kumuona hospitalini wakati Mobeto alipojifungua ndicho kilichomkera zaidi mzazi huyo.

Baada ya habari za Diamond kutembea na Mobeto kuvuma chini kwa chini kwa muda mrefu, kupitia vipande video vilivyorushwa na Shilawadu, vilimfanya Zari athibitishie pasi na shaka kwamba kweli Mobeto amezaa na Diamond.

TUENDELEE NA MAHOJIANO…

Ijumaa: Sasa inawezekana alishajua kosa lake ameamua kujirudi mama, huoni kama unapaswa kumsamehe?

Mama Diamond: Yaani kiufupi simpendi na simtaki na kila akikanyaga hapa kwangu ni kipigo tu.

Ijumaa: Kuna mtu yeyote alikutonya kuwa Mobeto yuko ndani siku ya tukio?

Mama Diamond: Ni kama zari tu. Mimi nafikiri kama mganga wake kamtuma aje anijaribu afike tena kwangu aone kama sitomfanya kitu kibaya.

Ijumaa: Kwa sababu gani lakini umfanyie kitu mbaya kwani kulala na Diamond ni kosa?

Mama Diamond: Alipokuja kiwizi usiku ule na kulala nyumbani kwangu, alipaswa kuondoka kabla sijamuona kwa nini alisubiri mimi nimkute maana siku hiyo asubuhi yake nilitoka na nilivyorudi ndipo nikamkuta.

Ijumaa: Ulivyomkuta ikawaje?

Mama Diamond: Mimi nilimsubiri tu getini na nilishajiapiza lazima nimpige.

Ijumaa: Sasa varangati lote Diamond alikuwa wapi?

Mama Diamond: Yupo na yeye ndiyo alimsaidia kumuamulia mimi nikabaki na wigi la sivyo ingekuwa shida.
Ijumaa: Kwa hiyo baada ya kubaki na wigi yeye alifanyaje?

Mama Diamond: Alikimbia na viatu mkononi, maana nilikuwa nimeshavitupa nje ya nyumba yangu.

Ijumaa: Kuna sababu nyingine kubwa ya kumchukia Mobeto?

Mama Diamond: Kwanza tu siyo mwanamke wa kuoa (wife material) hajui kutandika hata kitanda wala kufanya tu usafi ni shida.
Ijumaa: Ulimuona wapi mama hawezi kufanya hivyo vitu?

Mama Diamond: Si alishakaa hapa kipindi nipo Kigoma nilivyorudi ndani hakutamaniki kabisa.

Ijumaa: Lakini sasa huoni kama inaweza kuwa ni tatizo maana unaweza ukawa unamchukia lakini Diamond ndiyo kafika pale na ndio mtarajiwa wake?
Mama Diamond: Yaani atajua yeye mwenyewe maana mimi ndiyo nimemzaa Diamond na siyo yeye sasa sijui nani ana nguvu hapo.

Ijumaa: Je, Diamond akiamua leo kufumba macho na kumuoa Mobeto itakuwaje?

Mama Diamond: Siwezi kukanyaga kwenye hiyo harusi hata siku moja watasherekea wenyewe.

Ijumaa: Lakini pia si kuna madai wewe na mama Mobeto mlikuwa marafiki sana sasa kwa nini msilimalize hili kiutu uzima?

Mama Diamond: Hatujawahi kuwa marafiki hata siku moja maana mama Mobeto mwenyewe nilimuona kwenye bethidei yangu mara moja tu, hatuna uhusiano wowote kwanza mimi sina marafiki.

Ijumaa: Unaonekana unaposti sana picha za wajukuu zako ambao ni watoto wa Zari, unamzungumziaje Zari?

Mama Diamond: Ninamheshimu Zari kwa sababu ni mwanamke ambaye ndiyo wa kwanza kabisa kumfanya mwanangu aitwe baba.
Ijumaa: Kuna kipindi ilidaiwa kuwa ulimlisha keki Zari kwa mkono wa kushoto, unazungumziaje hiyo?

Mama Diamond: Maneno ya watu mitandaoni mimi ‘shoto’ ni mkono wangu ninaotumia siku zote.

Ijumaa: Una mpango gani wa kuhakikisha mwanao na Zari wanakuwa pamoja tena?

Mama Diamond: Hayo mambo ya kuwa pamoja ni wao wenyewe mimi ni kusubiri tu Nasibu anilete mwanamke anayejiheshimu, kujielewa na awe amempenda mwenyewe siyo huyu Mobeto.

Ijumaa: Vipi kuhusu Wema maana hivi karibuni ulimposti na kumsifia.

Mama Diamond: Nilimsifia kwa vile alipendeza na si vinginevyo maana mtu akipendeza lazima umpe sifa zake.

Ijumaa: Asante sana mama kwa ushirikiano.
Mama Diamond: Asante sana.

Baada ya kushiba maneno mazito kutoka kwa mama mzaa chema kama wasemavyo waswahili, Ijumaa lilimtafuta Mobeto ili naye alimegee chochote kitu kuhusu ishu ya kipigo kutoka kwa mkwewe lakini haikuwezekana kutokana na simu ya mrembo huyo kuita bila kupokelewa.

Hata hivyo, kwa kuwa ubuyu wa kipigo ulianza kitambo na ulikosa wa kuumung’unya vizuri, gazeti ndugu la hili, Amani lilifanikiwa kuzungumza na mama Mobeto wiki hii kuhusu tetesi za mwanaye kupigwa ukweni lakini alikanusha.

“Mama Diamond hawezi kumpiga mwanangu, Mobeto ni mtu mzima kwa hiyo hizo habari si za kweli,” haya ndiyo yalikuwa majibu ya mama Mobeto ambayo leo yanaonekana yalitaka kuficha moto na kusahau moshi ufukao.

Ijumaa bado liko kazini kumtafuta Mobeto ili kupata maelezo yake juu ya ishu ya kupigwa pamoja na tuhuma nyingine alizotoa mama Diamond eti kwamba hawezi kufanya hata usafi wa nyumba, kweli!

Stori:IMELDA MTEMA, DAR globalpb
xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx